Friday, February 19, 2016

a shule ya sekondari ya wasichana wenye vipaji ya Kilakala wakifurahia jambo wakati wa mahafali.
TUNAPOUANZA mwaka 2016, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa miongoni mwa majukumu yake mbalimbali, imejipanga kikamilifu kusimamia utekelezaji wa dhana ya elimu bila malipo.
Dhana hii inazingatia uendeshaji wa shule bila ada wala michango ya aina yoyote ya lazima kutoka kwa wazazi/walezi wa wanafunzi kama ilivyoainishwa katika ibara ya 3.1.5 ya Sera ya Elimu na Mafunzo (2014) na ibara ya 52(a) ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2015.
Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kupitia Waziri wa Nchi, George Simbachawene anabainisha kuwa Serikali imejipanga kugharamia uendeshaji wa shule ili kuziba pengo la ada na michango mbalimbali iliyokuwa inatolewa na wazazi na walezi. Anaeleza kuwa kwa kuanzia Serikali imetenga jumla ya Sh bilioni 131.4 ikiwa ni fedha za ruzuku ya uendeshaji wa shule, chakula, mitihani na fidia ya ada.
Fedha hizo zitapelekwa moja kwa moja shuleni kutoka Hazina kwa wastani wa Sh bilioni 18.777 kila mwezi kwa ajili ya: Ruzuku ya Uendeshaji wa Shule (Capitation Grants- CG) ya Sh 10,000 kwa mwanafunzi wa shule za msingi na Sh 25,000 kwa mwanafunzi wa sekondari kwa mwaka. Pia akaunti hiyo itapokea fedha za wanafunzi wa bweni ambapo Serikali itatoa Sh 1,500 kwa siku kwa mwanafunzi wa bweni wa shule za msingi na sekondari kwa ajili ya chakula; fidia ada ya Sh 20,000 kwa mwanafunzi wa kutwa na Sh 70,000 kwa mwanafunzi wa bweni wa kidato cha kwanza hadi cha nne kwa mwaka.
Mzazi hatatakiwa kulipa fedha za mitihani wala michango yoyote hivyo wazazi wanahimishwa kuwapeleka shule watoto wao ili waweze kupata elimu itakayowasaidia kukabiliana na changamoto za maisha. Anafafanua kuwa upo umuhimu wa kutoa elimu msingi bila malipo kwani kufanya hivyo kutaongeza kiwango cha uandikishaji kwa watoto wote wenye rika lengwa, kuimarisha mahudhurio ya wanafunzi na pia ufaulu wa wanafunzi katika mitihani mbalimbali utaongezeka.
Simbachawene anasema kuwa katika utekelezaji wa uendeshaji wa elimu msingi bila malipo imeainisha majukumu ya serikali kuhusu utoaji wa elimumsingi bila malipo kama yalivyoelezwa katika Waraka wa Elimu Namba sita wa mwaka 2015. “Majukumu hayo ni pamoja na kutafasiri sera kwa kutoa nyaraka, miongozo na kusimamia utekelezaji wake katika ngazi mbalimbali za kiutawala kuanzia wizara, mikoa, wilaya, halmashauri, kata na shule,” anaeleza Simbachawene.
Mikakati mingine iliyowekwa na Ofisi ya Rais, Tamisemi, katika mwaka 2016 ni kuhakikisha kuwa tatizo la upungufu wa madawati kwa wanafunzi shuleni linamalizika katika kipindi kijacho cha miezi sita. Simbachawene anasema hakuna sababu ya kukosekana kwa madawati shuleni, kwani, nchi ina misitu ya kutosha kwa ajili ya kutengeneza mbao na madawati, hivyo amewataka Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kushirikiana na Watendaji wa Halmashauri kuhakikisha tatizo hilo linamalizwa.
“Tunawaahidi Watanzania kuwa ndani ya miezi sita hakuna mtoto atakayekaa chini kwa kukosa madawati, nami sitakubali nikae mwaka mmoja na kushuhudia watoto wetu wanaaendelea kukaa chini kwa kukosa madawati,” Simbachawene. Waziri Simbachawene anayabainisha majukumu ya Ofisi ya Rais Tamisemi kuwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa mabadiliko wanayoyatarajia wananchi kutoka kwa serikali yao yanatekelezwa na hivyo anatoa wito kwa watumishi wa ofisi yake kuchapa kazi kuendana na kasi ya viongozi wao.
Anaeleza kuwa Watanzania wana matarajio makubwa na Serikali ya awamu ya tano, na akataka Mamlaka za Serikali za Mitaa ambazo ndizo zenye dhamana kubwa katika utoaji wa huduma mbalimbali za jamii kama vile kusimamia utekelezaji wa huduma za elimu bure kuanzia chekechea hadi kidato cha nne na kuhakikisha kuwa zinatolewa bure. Simbachawene anasema pamoja na utekelezaji na usimamizi wa shughuli za elimu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, wajibu mwingine kwa mamlaka hizo ni kusimamia shughuli za usafi wa mazingira katika maeneo yao ili kujikinga na maradhi kama kipindupindu.
Simbachawene anazipongeza halmashauri zote kwa namna ilivyoshiriki katika kufanikisha zoezi la kufanya usafi wa mazingira katika maeneo yao na hivyo kuitikia vyema mwito wa Rais Dk John Magufuli. Simbachawene anawataka wananchi wote kuuendeleza utamaduni wa kufanya usafi mara kwa mara na kwamba serikali kwa upande wake itahakikisha kuwa inaandaa mpango wa muda mfupi na mpango wa muda mrefu wa uzoaji taka katika makazi ya watu.
Anasema moja ya mikakati ya muda mfupi ni kuhakikisha kuwa taka zinazokusanywa hazikai muda mrefu katika makazi ya watu na kwamba ameziagiza halmashauri kuhakikisha kuwa zinaandaa utaratibu maalum kwa magari ya kuzoa taka kufanya kazi hiyo usiku. Waziri Simbachawene anasema mpango huo utarahisisha uzoaji taka kwa wingi na kwa haraka kwani usiku hakuna msongamano mkubwa wa magari kama ilivyo mchana na kwamba hatua hiyo itapunguza gharama na pia kuyawezesha magari hayo kufanya safari nyingi zaidi za kutupa taka hizo katika maeneo yaliyotengwa.
“Ili kurahisisha zoezi hilo kila mtaa unapaswa kutenga maeneo maalum ambayo wananchi watahifadhi taka hizo na pia kuchukuliwa kwa urahisi na magari ya kuzoa taka,” anasema Simbachawene. Waziri Simbachawene anaongeza kuwa ni wajibu wa kila mkazi katika familia kuhakikisha anazihifadhi taka katika eneo lililotengwa ili kutoleta bughudha kwa wakazi wengine.
Naibu Waziri Ofisi ya Rais anayeshughulikia Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Selemani Said Jafo, ametaka halmashauri zote nchini ambazo bado zinaendelea kukusanya mapato yake bila ya kutumia mfumo wa kielektroniki ziwe zimefanya hivyo kabla ya tarehe 10 Januari 2016. Jaffo anawataka Wakurugenzi wa Halmashauri nchini kuhakikisha kuwa agizo lake linatekelezwa na kuhakikisha kuwa mfumo huo unafanyakazi katika idara zote muhimu za halmashauri ikiwemo Utawala, Afya na Maliasili.
Anasema kuwepo kwa mfumo huo kutazisaidia halmashauri kuboresha ukusanyaji wa mapato na hivyo kuwa na ongezeko la fedha kwa ajili ya kutoa huduma muhimu kwa wananchi hasa kuboresha upatikanaji wa dawa katika zahanati na vituo vya afya vya halmashauri za wilaya. Jaffo anasema kuwa halmashauri zimekuwa zikikusanya mapato kidogo kutokana na kutokuwa na mfumo sahihi wa ukusanyaji mapato, na hivyo kuchangia mapato mengi kupotea mifukoni mwa watu.
Katika kusimamia utekelezaji wa majukumu yake kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa Naibu Waziri anazungumzia kero inayowakabili watumishi wa chini katika mamlaka hizo ambao hawapati mrejesho pindi wanapohitaji huduma mbalimbali katika halmashauri zao.
Anasema kumekuwa na mtindo kwa wakuu wa idara na Maofisa wa Halmashauri kutoshughulikia malalamiko ya watumishi wa chini hasa madai ya likizo za watumishi na kutopandishwa vyeo katika madaraja mbalimbali, hivyo anawaasa Wakurugenzi wa Halmashauri kwa kushirikiana na Maofisa Utumishi kuhakikisha kuwa kero hiyo inashughulikiwa mapema mwaka huu wa 2016.
Anasema endapo ataulizwa swali bungeni kuhusu kero na malalamiko yanayohusu watumishi kutolipwa madai ya likizo na kutopandishwa madaraja kwa watumishi wa ngazi za chini hapo atajua kuwa Mkurugenzi na Afisa Utumishi wa Halmashauri husika hawawezi kutimiza majukumu kulingana na nyadhfa walizopewa. “Unakuta mtumishi anafuatilia madai yake muda mrefu bila kupewa mrejesho, na hivyo kukosa muda wa kuendelea na majukumu yake katika kituo cha kazi.
Anasema vijiji vingi nchini tangu vifanye uchaguzi wa Serikali za Mitaa takribani mwaka mmoja uliopita havijafanya mikutano yake na matokeo yake wananchi wanachangishwa fedha wala kusomewa mapato na matumizi ya fedha hizo. “Nina taarifa kuwa vijiji vinkulishughulikia katika mwaka 2016 ni kuhakikisha kuwa viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa hususani Mameya na Wenyeviti wa Halmashauri wanapata mafunzo ya uongozi katika Chuo cha Serikali za Mitaa Hombolo kilichopo mkoani Dodoma".
Naibu Waziri amewapa maelekezo wakurugenzi wa halmashauri na manispaa nchini kuandaa utaratibu wa kuwapeleka wenyeviti na mameya kupata mafunzo ya kuwajengea uwezo ili waweze kufanyakazi kwa ufanizi zaidi. Akizungumza mara baada ya ziara yake ya kukitembelea chuo hicho, Jafo anasema kwa kuwa uchaguzi mkuu umepita na Madiwani wameshachaguliwa wanatakiwa wapewe mafunzo maalumu ya muda mfupi juu ya namna ya kusimamia na kuendesha halmashauri zao.
“Ninawaagiza Wakurugenzi wote wa Halmashauri kuwasiliana na Ofisi ya Rais, Tamisemi ili kujua namna ya kuwawezesha nauli Wenyeviti na Makamu Wenyeviti wa Halmashauri na Mameya na Manaibu Meya kuja Chuoni Hombolo kwa siku tatu au tano kupata mafunzo juu ya uendeshaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaam,” anasema Jaffo. Jaffo anaeleza kuwa ni vyema mafunzo hayo yatolewe kwa wenyeviti wa halmashauri, makamu wenyeviti, mameya na manaibu meya ili kuwajengea uwezo kwa madiwani wate wakiwezeshwa watakuwa na uelewa mpana wa masuala yanayohusu mikataba na malipo katika halmashauri zao.
Anasema kuwa gharama wanazotakiwa kuwezeshwa katika halmashauri zao ni nauli tu kwani na kusisitiza kuwa wakurugenzi hawatakiwi kuwalipa posho Wenyeviti hao wa halmashauri kwa kuwa kila kitu kinachohusu mafunzo hayo kitasimamiwa na Ofisi ya Rais Tamisemi kwa kushirikiana na Chuo cha Serikali za Mitaa Hombolo.
Kwa mujibu wa ibara ya 145 na 146 Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali za Mitaa ni vyombo vya haki na vyenye mamlaka ya kushiriki na kushirikisha wananchi katika kupanga na kutekeleza shughuli za maendeleo na utoaji wa huduma katika sehemu zao. Ofisi ya Rais-TAMISEMI ina wajibu wa kuzisimamia Mamlaka hizo ili ziweze kutekeleza majukumu yake kikamilifu. Mwandishi wa makala haya ni Ofisa Habari wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.

No comments:

Post a Comment