Friday, March 11, 2016

TWAWEZA yabaini Watanzania wana imani na mpango wa elimu bure.

Utafiti wa Taasisi ya Twaweza umebaini asilimia 88 ya Watanzania wanaimani na ahadi ya elimu bure kutekelezwa katika muda uliopangwa huku asilimia 76 wakiamini elimu hiyo kuwa na ubora zaidi.
Katika utafiti huo asilimia 15 wanaamini elimu bure haitaboresha elimu kutokana na ongezeko kubwa la uandikishwaji wa wanafunzi ambao utatumia rasilimali nyingi.
Matokeo hayo yametolewa na Twaweza kwenye muhtasari wa utafiti wenye jina la Mwanga Mpya kupitia takwimu zilizokusanywa kati ya Desemba 10, mwaka jana na Januari 2, mwaka huu kwa upande wa Tanzania Bara.
Pamoja na wananchi kuwa na imani na ahadi ya elimu bure wengi wamekuwa na mitazamo tofauti juu ubora wa elimu ya msingi katika kipindi cha miaka 10 iliyopita ambapo asilimia 49 wanasema ubora wa elimu umeongezeka na asilimia 36 wakibainisha kuwa elimu imezorota huku asilimia 14 wakisema hakuna mabadiliko yeyote.
Utafiti huo umebainisha kuwa wazazi wengi walikuwa wanaelemewa na michango ya shule ambapo wazazi na walezi 9 kati ya 10 huchangia elimu katika shule za umma.
Asilimia 89 ya wazazi wanakiri kulipa michango shuleni na asilimia 80 wakiripoti kulipa mpaka Sh50000 kwa mwaka huku asilimia 8 wakilipa zaidi ya Sh 100,000 kwa mwaka.
Utafiti huo pia umebainisha kuwa asilimia 37 ya wananchi wanaamini kuna uhusiano wa karibu kati ya jitihada za mwalimu na matokeo ya darasa la saba.

No comments:

Post a Comment